<?xml version="1.0" encoding="UTF-8"?>
<rdf:RDF xmlns="http://purl.org/rss/1.0/" xmlns:rdf="http://www.w3.org/1999/02/22-rdf-syntax-ns#" xmlns:dc="http://purl.org/dc/elements/1.1/">
<channel rdf:about="http://41.59.91.195:9090/handle/123456789/67">
<title>Thesis and Dissertation</title>
<link>http://41.59.91.195:9090/handle/123456789/67</link>
<description/>
<items>
<rdf:Seq>
<rdf:li rdf:resource="http://41.59.91.195:9090/handle/123456789/154"/>
<rdf:li rdf:resource="http://41.59.91.195:9090/handle/123456789/153"/>
</rdf:Seq>
</items>
<dc:date>2026-05-08T13:24:43Z</dc:date>
</channel>
<item rdf:about="http://41.59.91.195:9090/handle/123456789/154">
<title>Utohozi wa istilahi za kiingereza katika kiswahili: uchunguzi kifani wa taaluma za tiba na kompyuta</title>
<link>http://41.59.91.195:9090/handle/123456789/154</link>
<description>Utohozi wa istilahi za kiingereza katika kiswahili: uchunguzi kifani wa taaluma za tiba na kompyuta
Adolph, Editha
Kila lugha huwa na utaratibu wake wa ukuzaji na uendelezaji wa msamiati. Katika mchakato wa kupata msamiati wa lugha husika, mbinu mbalimbali hutumika. Utohozi ni mbinu mojawapo ambayo lugha huitumia katika kujitajirisha kimsamiati. Ili msamiati uweze kukubalika katika mbinu hii, kuna michakato mbalimbali inayopitiwa. Michakato hiyo huweza kusababisha athari katika lugha pokezi. Utafiti huu umechunguza utohozi wa istilahi za fani ya tiba na kompyuta za Kiingereza katika lugha ya Kiswahili kwa kuangazia michakato na athari zake. Utafiti umefanyika katika jiji la Dar es Salaam hususan katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kilichoko Wilaya ya Ubungo pamoja na Baraza la Kiswahili la Taifa lililopo Wilaya ya Kinondoni. Nadharia zilizoongoza utafiti huu ni Nadharia ya Fonolojia Zalishi (NFZ) iliyoasisiwa na Noam Chomsky na Morris Halle (1968) pamoja na Nadharia ya Mofolojia Leksika (NML) ambayo mwasisi wake ni Kiparsky (1982). Aidha, data ya utafiti huu ilikusanywa kwa kutumia mbinu za hojaji na uchambuzi wa matini. Data iliyokusanywa ilichambuliwa kwa kutumia mkabala wa maelezo na wa kitakwimu. Matokeo ya utafiti huu yameonesha kuwa lugha ya Kiswahili imetohoa istilahi za fani ya tiba na kompyuta  kutoka katika Kiingereza. Pia, utafiti umebaini kuwa wakati wa utohozi wa istilahi katika Kiswahili, michakato mbalimbali ya kifonolojia, kimofolojia na kisintaksia  hufanyika. Michakato hufanyika kadiri ya kanuni na taratibu za lugha ya Kiswahili ili istilahi ziweze kukubalika. Michakato ya kifonolojia iliyobainishwa katika utafiti huu ni pamoja na: mchakato wa udondoshaji, uchopekaji, usahilishaji wa irabu unganifu kuwa irabu sahili na mchakato wa ufupishaji wa irabu ndefu. Michakato ya kimofolojia  iliyoonekana kutokana na uchambuzi wa data ni pamoja na uambishaji ambao unafungamana na upangaji wa istilahi za Kiingereza katika ngeli za Kiswahili, uchakataji wa istilahi zenye muundo wa maneno ambatani. Kisintaksia, imebainika kuwa istilahi hutoholewa kwa kuhusisha mchakato wa kuchopeka vihusishi kati ya istilahi za Kiingereza. Halikadhalika, utafiti huu umebaini kuwa utohozi wa istilahi za fani ya tiba na kompyuta  za Kiingereza katika Kiswahili una athari chanya na hasi katika lugha ya Kiswahili. Athari chanya zilizobainika ni pamoja na zile za kifonolojia, kisemantiki na kileksika.  Athari za kifonolojia zilizoonekana katika utafiti huu ni pamoja na muundo mpya wa silabi katika Kiswahili, kuwapo kwa silabi funge katika Kiswahili na athari za kimatamshi zinazoambatana na ufifishaji wa sauti. Athari za kisemantiki zilizobainika ni pamoja na upatikanaji wa dhana za kisayansi pamoja na visawe vilivyotokana na utohozi. Kwa upande wa athari za kileksika, imedhihirika kuwa baadhi ya istilahi za fani ya tiba na kompyuta  zimeonekana kuongezeka katika Kiswahili. Athari hasi zilizobainika ni pamoja na zile za kimofolojia kisemantiki na kileksika. Kimofolojia imeonekana kuwa utohozi umesababisha muundo wa istilahi ndefu na zenye kutatanisha katika matamshi. Halikadhalika, matokeo ya utafiti huu yanaonesha kuwa kisemantiki kumezuka mfumuko wa visawe katika Kiswahili. Kileksika imebainika kuwa zipo istilahi za tiba na kompyuta zinazotumika mara chache. Utafiti huu unapendekeza kwamba, utohozi wa istilahi za lugha mbalimbali ufuate kanuni na taratibu zinazowekwa katika Kiswahili. Aidha, kuna haja ya wazungumzaji wa lugha ya Kiswahili kutumia istilahi za Kiswahili hata kama kuna istilahi mpya zinazotoholewa. Hivyo,  mtafiti anapendekeza kuwa pawepo na uhamasishaji wa matumizi ya istilahi za Kiswahili zilizopo ili kuepuka mfumko wa istilahi nyingi zinazorejelea dhana moja. Mtafiti anaona kuwa kuna haja ya kufanya uchunguzi zaidi kuhusu utohozi wa istilahi za Kiingereza katika Kiswahili  kwa miaka ijayo kwa kuwa ni bayana kuwa michakato ya utohozi ni endelevu.
PhD Thesis
</description>
<dc:date>2019-04-01T00:00:00Z</dc:date>
</item>
<item rdf:about="http://41.59.91.195:9090/handle/123456789/153">
<title>Utohozi wa nomino za kiswahili na athari yake katika ngeli za Kihaya</title>
<link>http://41.59.91.195:9090/handle/123456789/153</link>
<description>Utohozi wa nomino za kiswahili na athari yake katika ngeli za Kihaya
Adolph, Editha
Utafiti huu umechunguza utohozi wa nomino za Kiswahili katika Kihaya na athari yake katika ngeli za Kihaya. Utafiti umefanyika katika kata za Izigo, Mayondwe na Muhutwe wilayani Muleba mkoa wa Kagera nchini Tanzania. Kazi hii iliongozwa na Nadharia ya Mofolojia Leksika ya Kiparsky (1982). Aidha, data ya utafiti huu ilikusanywa kwa kutumia mbinu za hojaji, mahojiano, ushuhudiaji pamoja na njia za uwandani na maktabani. Halikadhalika, mkabala usio wa kiidadi ulitumika katika ukusanyaji na uchambuzi wa data ya utafiti huu.&#13;
&#13;
Matokeo ya utafiti huu yameonesha kuwa lugha ya Kihaya imekopa baadhi ya nomino kutoka katika Kiswahili. Baada ya nomino za Kiswahili kutoholewa katika Kihaya, zimefanyiwa michakato ya kifonolojia na kimofolojia kadiri ya kanuni na taratibu za lugha ya Kihaya ili ziweze kukubalika katika lugha ya Kihaya. Vilevile utafiti huu umebaini kuwa kuna  athari ya kingeli inayotokana na utohozi wa nomino za Kiswahili katika lugha ya Kihaya. Mfano, athari ya nomino za asili za Kihaya kubadili ngeli zake. &#13;
&#13;
Aidha, katika utafiti huu inapendekezwa kwamba uchunguzi ufanyike kuhusu mabadiliko ya ngeli yaliyotokea kuanzia zama za Mame-Bantu. Pia, mtafiti anapendekeza maeneo mengine yafanyiwe tafiti, mfano, uainishaji wa lahaja za Kihaya, fonolojia, semantiki, sintaksia na mofolojia ya Kihaya. Aidha, kuna haja ya kufanya uchunguzi tena kuhusu utohozi wa nomino za Kiswahili katika Kihaya  kwa miaka ijayo kwani ni wazi kuwa mchakato wa ukopaji  na utohozi ni endelevu.
M.A. Thesis
</description>
<dc:date>2014-10-01T00:00:00Z</dc:date>
</item>
</rdf:RDF>
